Boost

Baadhi ya kina mama hupata kitu kinachoitwa chuchu zilizopasuka wanaponyonyesha. Dalili ni pamoja na maumivu wakati wa kunyonyesha, kutokwa damu kwenye chuchu na kupasuka ngozi. Matatizo haya kwa kawaida ni matokeo ya mtoto wako kutonyonya kwa njia inayofaa.


Ikiwa una VVU na unanyonyesha ni muhimu kuzungumza na mtoa huduma wa afya haraka iwezekanavyo kuhusu matatizo yoyote ya chuchu zako, hasa ikiwa zinatoka damu. Hii ni kwa sababu chuchu zilizojeruhiwa zinaweza kuongeza uwezekano wa kumwambukiza mtoto wako VVU. Atakushauri jinsi ya kunyonyesha kwa usalama na kukusaidia jinsi ya kumbeba mtoto wako unapomnyonyesha ili kuepuka matatizo katika siku zijazo. Kumbuka kunyonyesha hakupaswi kuumiza.

Unapaswa pia kuwa mwangalifu wa uvimbe wa titi, hali ambayo matiti yako huvimba. Unaweza kugundua kuwa ni mekundu, yenye joto na maumivu. Hili pia ni jambo ambalo unapaswa kuzungumza na mtaalamu wa huduma ya afya kwani linaweza pia kuongeza hatari ya maambukizi ya VVU.  

Kwa angalau miezi sita ya kwanza unashauriwa kunyonyesha maziwa ya mama pekee. Hii ni kwa sababu tumbo la mtoto ni dhaifu sana katika miezi hii michache ya kwanza. Kumpa mtoto maziwa ya mama pamoja na vyakula vingine kunaweza kuathiri tumbo la mtoto wako. Ikiwa tumbo la mtoto wako limeathirika, yuko katika hatari zaidi ya kuambukizwa VVU. Ikiwa wewe au mtoto wako anaharisha au kutapika unapaswa kuzungumza na mhudumu wa afya, kwani hii inaweza kuwa ishara ya tumbo lililoathirika.

Ingawa mtoto wako hapaswi kutumia vyakula vingine, unaruhusiwa kumpa dawa zozote ambazo umeshauriwa. 

Unyonyeshaji huwapa watoto wako mwanzo mzuri kiafya maishani. Ilimradi unazingatia matibabu yako ya kupunguza makali ya VVU, unyonyeshaji ni chaguo salama na bora kwa mtoto wako.
Faida za kunyonyesha zinaweza kudumu kwa muda mrefu katika maisha ya mtoto zikiwa na matokeo bora kwa mama na mtoto. Baadhi ya faida muhimu zaidi ni:
1. Kunyonyesha huwapa kina mama na watoto wao fursa ya kuwa na uhusiano wa karibu. Wakati wa kunyonyesha, mama na mtoto hutagusana baina yao na kugusana kwa ngozi zao kunaweza kuwafanya wahisi kuwa karibu.
2. Kunyonyesha huwaruhusu kina mama kushiriki kingamwili zao na watoto wao. Hizi ni muhimu kwa kupambana na maambukizi na zinaweza kumlinda mtoto wako dhidi ya kuugua.
3. Maziwa ya mama yamejaa virutubisho na maji ambayo watoto wanahitaji ili kukua. Kunyonyesha huwalinda watoto wachanga dhidi ya hatari za utapiamlo na huwapa nguvu na vitamini wanazohitaji.
4. Kunyonyesha huwalinda watoto wachanga dhidi ya hatari za maji machafu, ambayo yanaweza kusababisha kuhara na matatizo mengine ya kiafya, ambayo yanaweza kuwa hatari.
5. Kunyonyesha ni kuzuri kwa afya ya mama. Hupunguza hatari ya wanawake kupata magonjwa fulani baadaye maishani, ikiwa ni pamoja na saratani ya ovari na matiti.